Mwanafunzi wa darasa la saba amejifungua wakati akifanya mtihani wa kuhitimu elimu ya msingi wilayani Muleba, Kagera.
Tukio hilo lilitokea juzi kati ya saa nne na tano asubuhi katika
Shule ya Msingi Kabiri katika Kijiji na Kata ya Kabirizi, Nshamba wakati
mwanafunzi huyo, mwenye umri wa miaka 14 (jina na namba yake ya mtihani
inahifadhiwa) akifanya mtihani wa pili na wenzake ndani ya chumba cha
mtihani.
Kwa mujibu wa habari zilizopatikana kutoka shule hiyo, mwanafunzi
huyo, alimwomba Msimamizi muda mfupi baada ya kuanza mtihani wa
Hisabati, amruhusu kutoka nje kwa kuwa alikuwa akijisikia vibaya.
Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali vya habari kutoka eneo la tukio,
baada ya mwanafunzi huyo kumwomba Msimamizi ruhusa, alimzuia akidhani ni
ujanja wa kutaka kwenda kuchukua majibu, lakini baadaye aliona
akijinyonganyonga.
“Msimamizi alimwuliza anaumwa nini akamwambia anaumwa tumbo na baada
ya kuendelea kumhoji alimweleza wazi kwamba anaumwa uchungu, hali
iliyomfanya Msimamizi aende kwa mmoja wa walimu wa shule hiyo na
kumwomba msaada,” alisema mmoja wa watahiniwa hao na kuongeza:
“Walimchukua na kumwingiza kwenye nyumba ya mwalimu huyo na kumfuata
mkunga wa jadi ambaye alimsaidia kujifungua salama mtoto wa kiume”.
Kwa mujibu wa chanzo chetu, mtoto huyo alipewa jina la OMR, mfumo
mpya maalumu unaotumika kujibu maswali ya mtihani wa darasa la saba
mwaka huu, ambapo mwanafunzi anaainisha jibu sahihi kwa kusiliba kwa
kalamu ya risasi.
Akizungumzia tukio hilo, Kaimu Ofisa Elimu wa Wilaya ya Muleba,
Savera Celestine alithibitisha binti huyo kujifungua, lakini hakutaka
kulizungumzia kwa undani suala hilo, kwa madai kuwa mzungumzaji mkuu wa
masuala yote ya mtihani ni Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya
Wilaya, “Ni kweli tukio hilo lipo, lakini mimi ndio nimefika hapa
ofisini sasa hivi, sijapokea taarifa rasmi juu ya tukio hilo, lakini
hata kama ningelikuwa nalo siwezi kulizungumzia kwa sababu anayepaswa
kuzungumzia masuala yote ya mtihani huu ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya
Wilaya, hebu mpigie atakupa taarifa,” alisema Kaimu Ofisa Elimu.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya hiyo ambaye pia ni
Mwenyekiti wa Kamati ya Mtihani ya Wilaya, Oliver Vavunge alipotafutwa
kwa njia ya simu ili kuzungumzia tukio hilo, hakukiri wala kukanusha
kuwapo tukio hilo na kusisitiza, kwamba atazungumza baada ya kupokea
taarifa ya wilaya nzima kuhusu mtihani huo, “Kwa sasa niko huku kisiwani
nashughulikia masuala ya mtihani, siwezi kuzungumzia jambo lolote la
mtihani, natarajia kufanya hivyo kesho (leo) ambapo nitakuwa nimepata
taarifa ya wilaya nzima, tena tutakuwa tumefanya majumuisho yote,”
alisema Vavunge.
Ofisa Mtendaji wa Kata hiyo, Ally Rajabu naye kwa njia ya simu,
alikiri kutokea tukio hilo na kueleza kwamba baada ya mwanafunzi huyo
kujifungua, alionekana kuchoka na walimtoa kwenye nyumba ya mwalimu na
kumpeleka kwao.
Alisema hata hivyo, alikuwa chini ya ulinzi wa askari waliokuwa
wakimsubiri apate nguvu ili ikiwezekana arejeshwe shuleni kuendelea na
mtihani, ambao alipaswa kumalizia Hisabati na kisha kufanya mtihani
mwingine wa Kiswahili ambao ulikuwa ukifuata.
Mkuu wa Wilaya, Lembris Kipuyo naye alithibitisha tukio hilo na
kueleza kuwa kwa mujibu wa taarifa alizopewa na vyombo vya ulinzi na
usalama kupitia Msimamizi wa Mtihani shuleni hapo, Christina Didas,
mwanafunzi huyo aliendelea na mtihani wa Hisabati na baadaye wa
Kiswahili ambao ulikuwa wa mwisho kwa juzi, “Ni kweli tumepatwa na tukio
hilo na taarifa rasmi nilizonazo ni kwamba baada ya mwanafunzi huyo
kujifungua salama, alipewa muda wa kupumzika na baadaye alirejea na
kufanya mitihani yake yote na nimeelezwa kwamba leo (jana) pia kama hali
yake itakuwa nzuri ataendelea na mitihani ya mwisho,” alisema Kipuyo
jana alipozungumza na gazeti hili kwa simu.