Na: Florence Majani,MWANANCHI
KWA wakazi wa Dar es Salaam, mawingu yanapotanda angani na
kutengeneza giza ambalo huashiria mvua, kwao huwa ni jambo la kawaida na
pengine ni ahueni kwa karaha za joto kali. Lakini kwa wakazi wa mkoa wa
Rukwa, ikiwemo hasa Sumbawanga, dalili ya mvua inayoambatana na radi ni
tishio la umauti, kwani mara nyingi radi hizi si za kawaida au za asili
bali ni za kichawi na hutengenezwa na wanadamu kwa madhumuni ya kuua.
Mkoa wa Rukwa hususani wilaya ya Sumbawanga, ni eneo linalosifika kwa
imani za kishirikina nchini. Lakini katika masuala ya utaalamu wa radi,
yapo maeneo na watu maalum ambao wana uwezo wa kutengeneza radi. Ukiwa
unatokea wilaya ya Sumbawanga kuelekea wilaya ya Nkasi, ndipo vilipo
vijiji maarufu kwa kutengeneza radi hizo.
Baadhi ya vijiji hivyo ni Sintale na Chipu, ambako ndiko walipo
wataalamu wenye uwezo na nguvu za ziada za kutengeneza radi. Kwa nini
radi zinatengenezwa? Radi hizi zinatengenezwa kwa ajili ya kuua au
kuwajeruhi maadui. Kwa mfano, kama yupo aliyekudhulumu, aliyekuibia mke
au mume, aliyekugonga na gari bila kukulipia gharama za matibabu au
anayekutusi na kukukebehi. Vijiji vya Sintale, Chipu na Kalundi,
vimepakana, kinaanza kijiji cha Kalundi kisha Sintale na cha mwisho ni
Chipu. Vijiji hivyo viko duni kimaendeleo na ukubwa.
Hata hivyo huku ndipo walipo watalaamu na mafundi wa kuunda radi.
Nilipokuwa mkoani humo hivi karibuni na mwenyeji wangu, tulielekezwa na
wenyeji wa Kalundi kwa mganga wa kwanza nayeitwa Mashaka ambaye
anaaminiwa kwa kuunda radi. Baada ya kufika kwa Mashaka, tunamkuta akiwa
na wateja kadhaa. Ninamweleza shida yangu na kumtonya kuwa ni shida ya
kipekee kidogo. Namweleza kuwa nahitaji kununua radi kwani nina adui
yangu aliyenidhulumu fedha nyingi. Mashaka anajibu kuwa yeye si mtaalamu
wa radi bali anatibu maradhi tu.
Anasema: “Lakini yupo mtaalamu wa radi, anaitwa mzee Chimwaga,
anaishi kijiji cha Sintale. Ngoja nimpigie simu sasa hivi,” Mganga huyu
anazungumza kwenye simu kwa lugha ya kifipa, na baada ya dakika chache
anakata simu na kutugeukia na kusema: “Yupo- nendeni- kutoka hapa kwenda
Sintale kwa Honda ni dakika 20, mkimuuliza yeyote, atawapeleka kwa mzee
huyo,” Kwa kuhofia muda, hatukwenda kwa mganga Mzee Chimwaga, na badala
yake tunakwenda eneo jingine na kuuliza iwapo kuna mganga mwingine
mwenye utaalamu wa radi. Mzee mmoja anatuelekeza kuwa yupo mganga
anayeitwa Ntoro, mwenyeji wa hapo hapo Kalundi ambaye naye ni mtaalamu
wa radi.
Tunaelekezwa kwa mganga Ntoro, tunapofika tunamkuta akiwa na wake
zake wawili na watoto wasiopungua wanane. Anatukaribisha na tunamweleza
shida yetu. Mganga Ntoro anasema, yeye hutengeneza radi lakini kwa
wakati ule alikuwa kaishiwa vifaa, hivyo aliamua kumpigia simu mganga
mwenzake mwenyeji wa kijiji cha Sintale ambaye ana ujuzi huo pia.
Anashika simu, na kumpigia mganga huyo tuliyebaini kuwa anaitwa
Maisha, huku akimsisitizia afike haraka azungumze na wateja. Wakati
tukimsubiri Mganga Maisha afike, tulianza kumdodosa Mganga Ntoro kuhusu
utaalamu huo wa kuunda radi. Ntoro anasema, kwa kawaida huduma ya radi
huuzwa, au hutozwa gharama kwa bei ya kuanzia Sh40,000 hadi 30,000 tu na
hiyo ni kulingana na umbali wa eneo alipo mtu anayetakiwa kuuwawa na
aina ya radi.
“Kwa mfano watu wanaotoka Zambia au Kongo tunawachaji fedha nyingi
zaidi kwa sababu ya umbali, lakini kwa maeneo ya karibu bei ni nafuu
kidogo,” anasema Ntoro. Radi hutengenezwaje? Ntoro anasema, kwa kabila
la kifipa, utaalam wa kuunda radi huitwa ‘Namasata’. Radi hutengenezwa
kichawi, lakini mtu yeyote anaweza kufundishwa na kuweza kuitengeneza,
ili mradi afuate masharti. Anasema zipo radi za aina tatu, ya kwanza ni
ya maji, ya pili ni ya pembe, na ya tatu ni ya gome la mti. Zote hizo
hutengenezwa kulingana na umbali na ubora wake.
“Radi ya pembe ni ya hatari zaidi, huchoma na kuweza kutekeza watu na
mali, na huenda umbali mrefu tofauti na radi ya gome la miti,” anasema
Huku tukiendelea kumdadisi, mganga Ntoro anasema, radi ya maji
hutengenezwa kwa kuchukua sahani mpya, bakuli mpya au chupa ya udongo.
Kisha mtaalamu huweka dawa ndani ya chupa au bakuli na kuisemea maneno
fulani.
“Ukishanuiza, unaviweka vifaa hivyo ndani, kesho asubuhi utakuta maji
ndani ya chupa au kama uliweka bakuli basi utaona maji ndani ya
bakuli,” anasema na kuongeza, “Baada ya hapo unachukua vifaa vile na
kuanza kunuiza adhabu unayotaka impate mbaya wako, kwa kumtaja jina.
Kama huna jina basi uwe na nyayo zake, nguo au kitu chake chochote
kile.”
Anasema baada ya kunuiza, unachukua bakuli au chupa ikiwa juu ya
sahani na kuyarusha maji yale juu, kwa nguvu za kichawi, maji yale
hupotea lakini kama kutakuwa na kasoro yeyote, maji yale humrudia
aliyeyarusha. Endapo mtaalamu atairusha radi ile kwa mtu asiye na
makosa, basi maji yatarudi chini na kama kweli mtu yule amefanya kosa,
basi maji hayatarudi na yatakwenda angani na kuanza kutengeneza wingu
jeusi linaloambatana na ngurumo.
“Maji yakisharushwa juu, baada ya saa moja tu, utaanza kuona angani
kiwingu cheusi na kizito sana, mvua inaweza kunyesha kidogo na kisha
ngurumo za kutisha … basi hapo ujue kazi tayari na mbaya wako
kashamalizwa,” anasema na kuongeza: “Kama unairusha radi kwa mtu asiye
na makosa kabisa, au ukakosea masharti radi inaweza kukurudia na
kukuunguza wewe.
Mtu akiniudhi mimi huwa nazirusha tu,” Radi ya pembe hutengenezwaje?
Wakati tukiendelea kumsubiri mganga Maisha, kutoka Chipu, Mganga Ntoro
anaendelea kutupa utaalamu huo bila kujua kuwa alikuwa akichunguzwa.
Sasa anasimulia namna ya kutengeneza radi ya pembe. Anasema, radi hii
hutengenezwa kwa pembe ya mbuzi au kondoo, ambayo kwa kawaida huwa na
uwazi katikati.
‘Tunachukua pembe, tunaweka dawa ndani yake, (yaani kwenye uwazi)
tunafunga hirizi kuizunguka pembe, pamoja na shanga, kisha tunanuiza
maneno kadhaa ya kichawi, na kisha tunairusha kuelekea alipo mlengwa,”
anasema Radi hii ni kama kimondo, inaporushwa, hupaa angani na hufuka
moshi katika upande wa mbele wa pembe wenye uwazi kama zifanyavyo ndege
za kushambulia(rocket). Mganga Ntoro anasema, radi hii huweza kupaa
umbali mrefu na huweza kuharibu mali, mifugo na binadamu ambaye
anawindwa.
Kuhusu namna ya kutengenez radi ya gome la mti, Ntoro anasema hiyo
ina masharti makali ambayo si rahisi kuzitoa siri zake kwa kila mtu.
Hata hivyo, baada ya muda mfupi, mganga Maisha anapiga simu na kusema
kuwa ameshindwa kufika kwa sababu ametingwa na shughuli za mazishi na
kutaka twende siku inayofuata asubuhi na mapema.
Mkazi mwingine wa kijiji hicho, David Ntare anasema mauaji ya radi ni
jambo la muda mrefu mahali hapo kwani wanaotumia uchawi wa radi
wamekuwa wakijigamba mitaani kwa uweza wao huo. “Tangu nazaliwa nasikia
vifo vya radi na nina uhakika si radi za kawaida kwa sababu, wanaokufa
mara nyingi huwa na uhasama na mtu, kama kumuibia mke,mume, kuiba au
kutukana,” anasema Ntare.
Ntare analihusisha tukio la kuungua kwa benki ya NMB, wilayani Nkasi,
tarafa ya Namanyere lililotokea miaka ya nyuma na uchawi wa radi. “Ile
benki iliunguzwa na radi na mzee mmoja mkulima wa kijiji cha Kizi baada
ya aliibiwa hela nyingi katika akaunti yake, akaona alipe kisasi kwa
njia ile. Ile benki iliungua wa radi, hakuna asiyejua,” anasema Inadaiwa
kuwa wenyeji wa hapa aghalabu huviona vitu hivi na hujua madhumuni yake
na mara nyingi vifo vya aina hii hutokea wilayani Sumbawanga. Anasema,
kwa kawaida mtu aliyeungua kwa radi huwa kama aliyeungua kwa umeme.
“Huungua na kuwa weusi kama mkaa, na wakati mwingine radi hukataa
kumuua mtu akiwa ndani, bali humrusha nje na kumchoma huko ili
isiwadhuru watu wengine,” anasema. Mwalimu wa shule ya msingi
Chalantala, Abeid Kisanga, anasema siku moja akiwafundisha wanafunzi wa
darasa la tatu somo la sayansi kuhusu radi , mwanafunzi wa kiume
alinyoosha kidole na kusema ‘mimi najua kutengeneza radi, baba
kanifundisha,”
Anjelo Singo, Afisa wa Polisi tarafa ya Namanyere anasema suala la
ushirikina wilaya ya Sumbawanga na Nkasi ni kubwa na yamekuwapo matukio
kadhaa ya vifo vinavyodaiwa kusababishwa na imani hizo. “Ingawa serikali
haiamini uchawi, lakini matukio ya radi yanayotokea hapa mengi ni ya
kishirikina, au matukio ya watu kuuwawa na kukatwa sehemu za siri
vilevile ni ya kishirikina,” anasema Anasema ni ukweli usiopingika kuwa
uchawi umesheheni katika maeneo haya na wakazi wake wameshaathirika
kisaiolojia kuhusu hilo.
Mkuu wa mkoa wa Rukwa, Mhandisi Stella Manyanya anasema ameshawahi
kusikia taarifa za kuwepo kwa wataalamu wa kuunda radi lakini akasema
hata hivyo hana uhakika nazo. “Unajua jiografia ya mkoa wa Rukwa imekaa
katika nyanda za juu, ni rahisi radi kulipuka maeneo haya. Hata hivyo
hili suala ni la kiimani zaidi,” anasema pamoja na mambo mengi
yanayosemwa kuhusu mkoa huo, kwa sasa maendeleo yanakwenda kwa kasi na
anaamini miaka michache ijayo, imani za ushirikina zitapungua kama sio
kwisha kabisa.